Tuesday, January 14, 2014

Plyum kocha mpya wa klabu ya Yanga

Hans Van Der Plyum ameingia mkataba wa kuinoa Young Africans kuanzia leo na moja kwa moja kesho mchana ataungana na wachezaji wake waliopo nchini Uturuki kwenye kambi ya mafunzo ya wiki mbili kujiandaa na mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom na mashindano ya kimataifa baadae.

Kocha huyo mwenye mafanikio makubwa nchini Ghana aliwasili nchini Tanzania juzi na leo kumalizana na uongozi wa klabu ya Young Africans kisha usiku huu kuanza safari ya kuelekea nchini Uturuki kuungana na timu yake mpya ambayo ipo katika kambi ya mafunzo kwenye jiji la Antlaya.

Uongozi wa Young Africans umefikia hatua hiyo baada ya kuridhika na wasifu na rekodi yake na kuwa kocha pekee aliyeweza kuushawishi uongozi na kumpa kazi kutoka katika maombi mengi ambayo yalikuwa yametumwa na yakiendelea kumiminika kuomba ajira katika klabu kongwe nchini Tanzania.

Kuajairiwa kwa mholanzi Hans Van Der Plyum kunafunga mjadala juu ya nani anakua mrithi wa Ernie Brandts ambaye alisitishiwa mkataba wake mwishoni mwa mwaka jana na kumalizana na uongozi wa klabu ya Yanga kabla ya kurejeja kwao nchini Uholanzi.

Akiongea na mtando rasmi wa klabu ya Young Africans SC mwenyekiti wa kamati ya mashindano Abdallah Bin Kleb amesema kwa pamoja wamekubaliana baada ya kurizika na uwezo na rekodi yake ambayo wanaamini itasaidia kuipeleka timu katika hatua nyingine.

Sisi tumeamua kuingia mkataba na kocha Van der Plyum ili aweze kuisaidia timu yetu kutoka katika hatua iliyo na kwenda mbele zaidi, mtazamo wetu mkubwa ni katika mashindano ya kimataifa hasa Klabu Bingwa kwa kushirikiana na kocha msaidizi mzoefu mwenye elimu ya juu pia ya ukocha nchini Mkwasa tunaamini tufanya vizuri katika Ligi Kuu na Klabu Bingwa Afrika.

Aidha Hans Van der Plyum amesema anashukru uongozi wa Young Africans kwa kumuamini na kumpa nafasi hiyo na kuahidi kwa kushirikiana na kocha Mkwasa na Pondamali ambao atakutana nao Uturuki watakiimarisha kikosi na pindi kitaporejea nchini kitakua katika hali nzuri na kucheza soka safi.

Pia kocha huyo mholanzi amesema anamjua vizuri kocha mkuu wa Simba SC Zdravko Logarusic kwani mwaka 2011 alikua akifundisha timu ya Ashanti Gold SC nchini Ghana na walipokutana katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya timu yake ya Berekum Chelsea aliweza kuibuka mbabe kwa kuifunga timu ya Ashanti mabao 4-0.

No comments:

Post a Comment